Na. Immaculate Makilika -MAELEZO
Wabunge nchini Rwanda wamepitisha kwa kauli moja muswada wa sheria ya kuifanya lugha Kiswahili kuwa lugha rasmi nchini humo.
Kufuatia
hatua hiyo, sasa Kiswahili nchini Rwanda kinakuwa moja kati ya lugha
tatu za Kinyarwanda, kiingereza na kifaransa zinazozungumzwa na wananchi
kama lugha rasmi miongozi mwao na kukifanya Kiswahili kuwa lugha ya nne
nchini humo.
Lugha ya Kiswahili nchini Rwanda inatazamiwa kuanza kutumika katika shughuli za uongozi na katika nyaraka za kiofisi.
Aidha, Waziri wa Michezo na Utamaduni nchini
Rwanda, Julienne Uwaci alisema kuwa uamuzi huo umefikiwa kutokana na
lugha hiyo kuwa na wazungumzaji wengi katika nchi za Jumuiya ya Afrika
Mashariki hivyo kuweza kurahisisha ushirikiano katika sekta mbalimbali
za maendeleo.
Aliongeza kuwa, “Kiswahili
ni lugha rasmi ambayo nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki
wanatakiwa kuitumia kwa kuwa kitaongeza tija kwa nchi ya Rwanda kufaidi
matunda ya utengano wa kiuchumi”
Wabunge mbalimbali wa nchi
hiyo wametoa maoni, akiwemo mbunge Jean Baptiste Rucibigango ambapo
alisema kuwa “Kiswahili ni lugha inayozungumzwa na watu wengi katika
ukanda wa Afrika Mashariki na hakika itakuwa na faida kuzungumzwa nchini Rwanda”.
Kiswahili kuwa lugha rasmi katika
nchi za ukanda wa Afrika Mashariki, kunaleta faida nyingi ikiwemo
kuongeza wigo wa shughuli za kibiashara na kukuza uchumi wa nchi
wananchama ambazo ni Tanzania, Kenya, Rwanda, Uganda, Burundi na Sudani
ya Kusini, pamoja na kuimarisha ushirikiano na mahusiano ya kidiplomasia
baina ya nchi hizi.
Hatua hiyo ya Rwanda
kuifanya lugha ya Kiswahili kuwa lugha ya rasmi ya Taifa ni fursa ya
adhimu kwa nchi jirani zinazozungumza zaidi Kiswahili ikiwemo Tanzania,
kwani itasaidia raia wake kuwa na nafasi murua kushiriki katika shughuli
za kibiashara na elimu.
mwisho
0 comments:
Post a Comment